WAKINAMAMA WAHIMIZWA KUENDELEA KUNYONYESHA WATOTO WAO

1
Afisa Lishe kutoka Kitengo cha Lishe Wizara ya Afya Fatma Ali Said akizungumza na waandishi wa habari kuhusu wiki ya unyonyeshaji katika ukumbi wa Wizara hiyo Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
(Picha na Ramadhani Ali)
………………………………………………………………………….
Na Ramadhani Ali-Maelezo Zanzibar
Akinamama wamehimizwa kuendelea kunyonyesha watoto wao maziwa ya kifua pekee katika kipindi cha miezi sita ya mwanzo bila ya kuwapa chakula chengine ili kuwajenga katika afya bora na kukua vizuri kiakili na kimwili.
Afisa Lishe kutoka Kitengo cha Lishe Wizara ya Afya Fatma Ali Said ameeleza hayo katika ukumbi wa wizara hiyo Mnazimmoja alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji iliyoanza jana.
Alisema maziwa ya mama pekee katika kipindi cha miezi sita ya mwanzao yanamkinga mtoto na maradhi mengi kwani yanavirutubisho vya kutosha vya kuwawekea kinga na kujenga upendo baina yake na mama.
Afisa huyo alisema mama anaponyonyesha mtoto  kipindi hicho bila kumpa kitu chengine inapunguza kutoka damu nyingi  katika siku 40 baada ya kujifungua na humsaidia kurudi katika hali yake ya kawaida kwa haraka.
Alikumbusha kuwa  kunyonyesha mtoto maziwa ya kifua pekee katika miezi sita ya mwanzo hakuna  gharama  kwa wazazi na baadhi ya akinamama inawasaidia kujiepusha na mimba nyengine  katika kipindi hicho na kupelekea uzazi wa mpango.
Alisema  bado jamii kubwa ya Wazanzibari haina mwamko wa kunyonyesha  maziwa ya mama pekee miezi sita ya mwanzo na utafiti uliofanywa mwaka jana unaonyesha  ni asilimia 20 tu ya akinamama ndio wanaonyonyesha  kwa  kutumia utaratibu huo.
Aliongeza kuwa madai ya baadhi ya watu kwamba maziwa ya mama pekee bila chakula chengine hayamtoshelezi mtoto hayana ukweli iwapo mtoto atanyonyeshwa kwa muda unaotakiwa.
Alisema mtoto anatakiwa anyonye kwa dakika zisizopungua 20 bila kupumzika ili apate maziwa yalioko mbali ambayo ndio yenye chakula na mafuta kwa ajili ya kumjenga mtoto.
“Maziwa ya mwanzo ya mama yanamaji mengi lakini  maziwa yanayochelewa kwa dakika 20 yanavirutubisho vyote muhimu katika makuzi ya mtoto,” aliongeza Afisa Lishe.
Aliwataka akinamama wanaofanyakazi  sehemu mbali mbali kufanya juhudi ya kuwakamulia maziwa watoto wao na kuyahifadhi vizuri ili waweze kupewa wakati hawapo majumbani.
Aidha aliwakumbusha akinamama kuendelea kunyonyesha watoto wao iwapo itatokea bahati ya kupata mimba nyengine wakati mtoto aliezaliwa bado anaumri mdogo kwani maziwa ya mama mjamzito hayana madhara yoyote kwa mtoto.
Kilele cha wiki ya unyonyeshaji kitakuwa tarehe 7 mwezi huu katika Wilaya ya Micheweni na kauli mbiu ya mwaka huu Tudumishe unyonyeshaji kwa pamoja.

Maoni