GAZETI LA MwanaHALISI LAPEWA SAA 24 LIOMBE RADHI

images
Dodoma, Jumatatu, Januari 30, 2017: Katika toleo la Jumatatu, Januari 30-Februari 5, 2017 gazeti la MwanaHALISI linalochapishwa na kampuni ya Hali Halisi Publishers LTD kumechapisha habari kuu katika ukurasa wa kwanza inayosomeka “Ufisadi ndani ya ofisi ya JPM.”
Licha ya habari hiyo kujenga dhana kuwa Rais John Pombe Magufuli anahusika na kilichoitwa ufisadi, msingi wa taarifa husika ni tatizo la manunuzi katika Shirika la Elimu Kibaha!
Kwa kuwa ni jambo lililodhahiri kuwa Shirika la Elimu Kibaha si ofisi, idara wala kitengo “ndani ya ofisi ya JPM” mwandishi na mhariri wa habari husika wamedhihirisha malengo ya kumchafua Rais binafsi kwa jamii.
Aidha, katika siku za karibuni Serikali imejitahidi kufanya mazungumzo na wahariri wa gazeti hili kwa lengo la kukumbushana maadili ya uandishi wa habari, ni bahati mbaya kwamba wamekuwa wakikaidi japo wito tu.
Kwa sababu hizi, Serikali inawaagiza wahariri wa gazeti hilo kujitathmini na kuchukua hatua kwa kutumia kifungu cha 40 cha Sheria ya Huduma za Habari, 2016 kinachowapa fursa ya kuomba radhi, kwa kumuomba radhi Rais ndani ya saa 24 kuanzia saa 10 jioni ya leo Januari 30, 2017.
Iwapo wahusika wataona muhali kufanya hivyo, Serikali itachukua hatua kali kwa mujibu wa sheria na masharti ya usajili ya gazeti husika. Tunaendelea kuwashukuru wanahabari wanaofuata maadili ya taaluma.
Imetolewa na:
Dkt. Hassan Abbasi,
Mkurugenzi Idara ya Habari-MAELEZO

Maoni