Baadhi ya wananchi waliotembelea Maonesho ya ‘Azam World of Cakes Exhibition’ wakipita kuangalia keki. |
JOPO la Majaji watatu na mabingwa
wa fani za mapishi leo wamewatangaza mabingwa wa utengenezaji keki
waliojitokeza katika Maonesho ya bidhaa za keki ‘Azam World of Cakes
Exhibition’ yaliofanyika katika Hoteli ya Serena ya jijini Dar es
Salaam.
Jumla ya makampuni na watengenezaji keki wapatao 39 wameshiriki
katika maonesho hayo ya keki yalioandaliwa na kampuni ya Insights
Productions Limited kwa udhamini wa Kampuni ya Azam Tanzania.
Akitangaza washindi katika
maonesho hayo ya keki, mmoja wa majaji ambaye pia ni Mpishi Mkuu, toka
Ramada Encore ya jijini Dar es Salaam, Edward Mukabana alisema timu ya
majaji hao imewapata washindi wa kwanza watatu katika makundi matatu;
yaani mshindi wa Keki yenye Radha Bora, Mbunifu Bora wa Keki na Mshindi
wa Keki yenye Mvuto Kimuonekano.
Jaji huyo wa ‘Azam World of Cakes
Exhibition’ aliwataja Amina Salim kuwa ndiye aliyeibuka mshindi wa keki
yenye radha bora zaidi, huku kampuni ya Beta Bakery ikitwaa taji la
mbunifu Bora wa Maonesho hayo ya keki. Pia alimtangaza Janeth Muawiriro
kuwa ndiye mshindi wa keki yenye Mvuto kimuonekano katika washiriki
wote.
Jopo hilo la majaji wa ‘Azam World
of Cakes Exhibition’ pia lilimtangaza Leila Dhiyebi kuwa ni mshindi wa
kwanza aliyepigiwa kura na wananchi waliotembelea maonesho hayo makubwa
ya keki Tanzania. Kundi lingine la washindi ambao keki zao ziliwavutia
majaji ni pamoja na Haika Shao na Caroline Gul pamoja na wanae wawili
ambao walishiriki kubuni umbo la keki kwa mchoro iliyotengenezwa na
mamayao.
Akizungumza awali kabla ya
kuwatangaza washindi, Jaji Mkuu wa Mashindano hayo ya ‘Azam World of
Cakes Exhibition’, Tom Owino (Excetive Chef) alisema walisema
wamezipitia keki zote za washiriki kuangalia vigezo mbalimbali vya
upishi, muonekano na kuonja radha ya kila keki kabla ya kukaa chini na
kuanza kufanya maamuzi ya pamoja ya majaji kwa kuzingatia vigenzo vya
msingi katika utengenezaji keki.
Aidha kwa upande wake, Marion
Elias Mkurugenzi wa Kampuni ya Insights Productions Limited, ambaye pia
ni Mratibu wa maonesho hayo alisema maonesho hayo yamekuwa na mvuto
baada ya kushirikisha makampuni na watu binafsi huku yakilenga kutangaza
bidhaa nzima ya keki na ubunifu katika utengenezaji.
Alisema washiriki wote wamepata
fursa ya kubadilishana uzoefu na kujifunza ubunifu zaidi wa shughuli
hizo toka kwa wataalam wengine jambo ambalo litawabadili kwa namna
fulani, ikiwa ni pamoja na kupata zawadi toka kampuni ya Azam na vyeti
maalum vya kutambua mchango wao kiushiriki.
Kwa upande wake Mratibu wa
Matangazo na Uhusiano wa Umma toka Kampuni ya SSB, Mohammed Ramadhan
alisema Azam ikiwa ni kampuni inayotengeneza unga bora wa kutengenezea
keki imeamua kudhamini ikiwa ni ishara ya kutambua taaluma hiyo ya
utengenezaji wa keki nje na ndani ya Tanzania. Wananchi walipata fursa
ya kuangalia keki mbalimbali pamoja na kuonja radha zake jambo ambalo
lilileta mvuto zaidi kwa washiriki.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
Maoni
Chapisha Maoni