WAKUU WA MIKOA KUJADILI AJIRA NCHINI

KONGAMANO la wakuu wa mikoa kuhusu ajira linatarajiwa kufanyika kwa siku mbili mkoani hapa kuanzia leo likishirikisha watu zaidi ya 200, imefahamika.

Madhumuni ya kongamano hilo ni kuwakutanisha wakuu wa mikoa na wadau mbalimbali kujadili kuhusu changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana na kupendekeza mikakati ya kukuza fursa za ajira nchini.

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudentia Kabaka aliwaambia waandishi wa habari jana mjini hapa kuwa kongamano hilo limeandaliwa na wizara yake kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani (ILO) na Taasisi ya Utafiti wa Masuala ya Uchumi na Kuondoa Umasikini (REPOA).

Kabaka alisema wajumbe zaidi ya 200 wakiwamo wakuu wa mikoa yote ya Tanzania Bara, makatibu tawala wa mikoa, wadau wa maendeleo, wakuu wa taasisi za umma na zisizo za kiserikali, sekta binafsi na vikundi vya vijana, watashiriki kongamano hilo.

“Kongamano hili la kitaifa litafanyika tarehe 19 na 20 Novemba, katika Ukumbi wa Mtakatifu Gaspar na litafunguliwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Pinda,” alisema Kabaka.

Alisema wakuu wa mikoa wataandaa na kusaini Azimio la namna watakavyosimamia utekelezaji wa mikakati ya kukuza uchumi kwa vijana nchini pamoja na mwongozo wa utekelezaji.

Alisema kaulimbiu ya Kongamano hilo ni “Ni wakati wa kuwawezesha vijana,” ikiwa na maana sasa si wakati tena wa kupanga kufanya nini, bali kuwawezesha vijana kwa kutumia fursa zilizopo katika maeneo yao.

 “ Katika kongamano hilo, mada mbalimbali zitawasilishwa na kujadiliwa na hatimaye kuandaa mikakati ya kukuza fursa za ajira ambayo itakuwa ni sehemu ya Azimio la Wakuu wa Mikoa,” alisema Kabaka.

Maoni