WABUNGE jana waliungana bila kujali
vyama vyao, kutetea kuwasilishwa bungeni na kujadiliwa kwa ripoti ya sakata la
uchotaji fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow baada ya kuwapo kwa taarifa kuwa
Mahakama imezuia.
Katika kile kilichoonekana kuwa
wabunge wanataka mbivu na mbichi za sakata hilo ziwekwe hadharani, walisema
hatua yoyote ya kuzuia suala hilo lisijadiliwe, inaweza kulivuruga Taifa na wao
kulaumiwa.
Hata hivyo, Waziri Mkuu Mizengo
Pinda alitoa angalizo kuwa ni vyema kuwapo kwa utulivu na kila mhimili
kusimamia mamlaka yake, na busara kutumika.
Bunge liliingia katika mjadala baada
ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), kuomba ufafanuzi
kutokana na kauli ya Waziri Mkuu wakati wa kipindi cha Maswali ya Papo kwa
Hapo.
Akijibu swali la Mbunge wa Mbozi
Magharibi, David Silinde (Chadema), Waziri Mkuu Pinda alisema yeye kama
Mwanasheria ingawa si Mwanasheria Mkuu, kuna kesi zaidi ya 10 mahakamani kuhusu
hilo, hivyo si vyema kuanza mjadala utakaotibua suala hilo.
Alisema hiyo si mara ya kwanza kwa
Bunge kutoshughulika na suala linaloendelea mahakamani.
Kauli hiyo ndiyo iliyomsimamisha
Kafulila na wabunge wengine wawili, Esther Bulaya (Viti Maalumu – CCM) na Moses
Machali (Kasulu Mjini – NCCR- Mageuzi), huku Kafulila akitaka uhakika wa kauli
ya Waziri Mkuu kama ripoti hiyo itapelekwa bungeni kujadiliwa au la.
Kutokana na hali hiyo, Naibu Spika
alitoa fursa kwa wabunge kadhaa kulijadili suala hilo kwa nia ya kumsaidia
kufikia maamuzi, lakini wote waliosimama ukiondoa Waziri Mkuu, walitaka ripoti
ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), iwasilishwe bungeni na
ijadiliwe.
Kwa sasa, ripoti hiyo inafanyiwa
uchambuzi kwa njia ya uchunguzi na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za
Serikali (PAC) chini ya Kabwe Zitto, kabla ya kuwasilishwa bungeni.
Wa kwanza kumshauri Naibu Spika
alikuwa Kafulila aliyesema kuwa suala hilo ni mtihani kwa Bunge, na ili nchi
isiingie katika machafuko, ripoti hiyo haina budi kuwasilishwa ndani ya Bunge.
“Bunge ndicho chombo chenye mamlaka
ya mwisho katika nchi, watu watatupima kama tunatosha kuisimamia Serikali kwa
jinsi tutakavyoshughulikia suala hili. Bunge lazima liheshimiwe, hatuwezi
kuwalinda watu wachache. Hiki ni kipimo cha uhalali wetu,” alisema.
Bulaya alisema Bunge lazima
liheshimiwe, na kwamba “CCM haiwezi kukubali kuchafuliwa na watu wachache, kila
mtu ale kwa urefu wa kamba yake. Ujangili, dawa za kulevya, Escrow marufuku.”
Naye Mbunge wa Longido, Michael
Laizer (CCM), licha ya kukiri kuwa miongoni mwa wasiolifahamu vyema suala hilo,
lakini alisema ni busara likajadiliwa na Bunge.
“Mimi silielewi vizuri, lakini ni
jambo kubwa linaloumiza vichwa. Kuna minong’ono mingi, kuna orodha inatajwa ya
wezi, hawajulikani ni kina nani, wengine wamo humo ndani. Naibu Spika tusifiche
wezi, kila kitu kiwekwe waziwazi, tuelewe, wengine wanapiga siasa. Ije ripoti
haraka, waliokula tuwaseme, halitupi raha,” alisema Laizer.
Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji
Peter Msigwa (Chadema), alisema ni vyema ripoti ikawasilishwa ili kujua mwizi
ni nani na kila mtu abebe msalaba wake.
“Huu ndio wasaa wa ukweli, wasaa wa
uamuzi. Hapa kuna watu waliitana tumbili na mwingine mwizi. Sasa ni wakati
mwafaka kujua mwizi ni nani na tumbili ni nani,” alisema Msigwa.
Naye James Lembeli wa Jimbo la
Kahama (CCM), alisema kama Operesheni Tokomeza ilikwenda na baadhi ya mawaziri,
kuna kigugumizi gani katika Escrow.
“Kila mtu atahukumiwa kwa matendo
yake, kama ni mtego basi uteguliwe. Historia itakukumbuka Naibu Spika kwa jinsi
utakavyoshughulikia suala hili,” alisema.
Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia
(NCCR- Mageuzi), alisema lazima kuwapo na uadilifu na uaminifu, hivyo waliohusika
na sakata hilo waende na maji, nchi itulie.
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu
Lissu (Chadema), akizungumza kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, alisema
Mahakama haiwezi kulifundisha kazi Bunge wala kulielekeza nini cha kufanya
kwani haina mamlaka hayo.
“Kama Bunge la Tisa linakumbukwa kwa
jinsi lilivyoshughulika na suala la Richmond, Bunge hili litakumbukwa kwa suala
hili la Escrow. Ripoti iletwe hapa, wa kusuka na kunyoa tumjue,” alisema Lissu.
Akizungumzia maendeleo ya kazi yao,
Zitto ambaye ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, alisema wako tayari kuiwasilisha
ripoti yao bungeni.
“Sisi hata kesho (leo) tunaweza
kuiwasilisha bungeni. Jana tumewahoji CAG, Takukuru na TRA na wamemaliza kazi
yetu. Rasimu ya kwanza inaandaliwa leo (jana) na kesho inaweza kuingia bungeni,
tukalijadili hili ili liishe,” alisema Zitto.
Hata hivyo, Waziri Mkuu Pinda
alisema si kazi ya Mahakama kuficha uozo, lakini ni muhimu kila mhimili wa Dola
ukatenda mambo kwa mujibu wa Katiba.
“Hata mimi nataka yajadiliwe yaishe,
lakini tutumie busara kubwa ili kuondoa mwingiliano na chombo kingine cha
maamuzi kama inavyotakiwa,” alisema.
Akihitimisha mjadala wake, Naibu
Spika Ndugai alifanya rejeo la kauli ya aliyekuwa Spika wa Bunge la Tisa,
Samuel Sitta akisema; “tukiwa viongozi hatuwezi kutengeneza umoja katika uozo.”
Ndugai alisema kwa kutazama hali ya wabunge ilivyokuwa jana wakati wa
kumshauri, aliahidi kuwa “tutatenda haki katika jambo hili.”
Maoni
Chapisha Maoni