MAANDALIZI YA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA YAMEKAMILIKA.

SERIKALI imesema maandalizi kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika kote nchini Desemba 14, mwaka huu, yamekamilika ikiwa ni pamoja na kusambazwa kwa masanduku ya kupigia kura na kwamba unatarajiwa kugharimu Sh bilioni 20.

Aidha, katika mchakato huo, vyama vya siasa vitaruhusiwa kuweka mawakala wao na gharama za mawakala zitalipwa na vyama husika.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa Idara ya Serikali za Mitaa katika Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Khalist Luanda alisema maandalizi ya uchaguzi huo yamekamilika.

Alisema gharama za uchaguzi huo, zinahusisha utengenezaji wa masanduku, kusafirisha masanduku hadi kwenye vituo vya kupigia kura, kusambaza vifaa na fomu mbalimbali pamoja na gharama za usimamizi wa uchaguzi huo hadi utakapokamilika.

Alisema Waziri Mkuu ndiye aliyepewa madaraka ya kutunga kanuni za kusimamia uchaguzi huo na tayari kanuni hizo zimewekwa kwenye mtandao wa wizara.

“Tayari masanduku ya kupiga kura yamesambazwa kwenye halmashauri zote nchini pamoja na fomu mbalimbali na vifaa vyote kwa ajili ya uchaguzi viko tayari,” alisema.

Alisema uandikishaji wa wapiga kura, utafanyika kwa kutumia Rejesta ya Wakazi, badala ya kutumia Daftari la Kudumu la Wapigakura ambalo linatumika katika uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani.

Alisema sababu kubwa ya kutotumia daftari la kudumu la wapiga kura ni kwa kuwa daftari hilo limeandaliwa kwa kuzingatia ukazi wa watu, mwisho katika ngazi ya kata.

Alisema uandikishaji utafanyika kwa kuwaorodhesha wakazi wenye sifa za kupiga kura kwenye rejista, zitakazokuwa katika vituo vya kuandikishia wapiga kura na vituo hivyo vitaandaliwa na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi.

Pia, alisema uandikishaji wa orodha ya wapigakura, utafanyika kwenye majengo ya umma na pale ambapo hakuna jengo la umma, uandikishaji utafanyika kwenye sehemu ambayo msimamizi msaidizi wa uchaguzi, atakuwa amekubaliana na viongozi wa vyama vya siasa.

Alisema wanaoruhusiwa kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea ni wale walio na umri kuanzia miaka 21; na wenye umri wa miaka 18 hawataruhusiwa kugombea, wao watabaki kuwa na sifa ya kuwa wapiga kura.

Mkurugenzi huyo alisema wasimamizi wa uchaguzi, wataandaa fomu za kugombea na kila fomu itakuwa na nembo ya halmashauri na nembo ya chama cha siasa chenye wagombea.

Alisema kila msimamizi wa uchaguzi, atahakikisha zinakuwepo fomu za kutosha za wagombea kwa uchaguzi wa viongozi wa vijiji, mitaa na vitongoji kulingana na nafasi zinazogombewa na fomu hizo zitatolewa bila masharti au malipo yoyote.

Alisema kutatolewa nakala mbili kwa kila ombi la mwombaji, nakala moja ya fomu baada ya kujazwa na mgombea na baada ya uteuzi itabandikwa nje kwenye ubao wa matangazo ili mgombea yeyote mwenye pingamizi ajitokeze; na nakala ya pili itabaki ofisini kwa msimamizi msaidizi wa uchaguzi kwa ajili ya kutunza kumbukumbu.

Pia, msimamizi wa uchaguzi kwa maana ya mkurugenzi wa mamlaka ya Serikali za Mitaa, atateua Ofisa wa umma ambaye ataandikisha na kuandaa orodha ya wapigakura katika kitongoji kwa ajili ya uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, wajumbe wa halmashauri ya kijiji na mwenyekiti wa kitongoji siku 21 kabla ya siku ya uchaguzi, ambayo ni Novemba 23, mwaka huu.

Alisema uandikishaji wa wapiga kura utafanyika kwa siku saba kuanzia Novemba 23 hadi Novemba 29, mwaka huu.

Alisema msimamizi wa uchaguzi atabandika orodha ya wapigakura mahali pa matangazo ya uchaguzi Novemba 30, mwaka huu na kutunza kumbukumbu yake.

Pia, orodha ya mwisho ya wapiga kura itabandikwa siku tatu kabla ya siku ya uchaguzi, ikiwa ni kuanzia Desemba 11 hadi Desemba 13, mwaka huu.

Maoni