DAFTARI LA WAPIGAKURA KUKAMILIKA APRILI 18.

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza rasmi kuanza kuboresha Daftari la Wapigakura kuanzia mwezi ujao na kwamba itakamilisha kazi hiyo Aprili 18 mwakani.

Kwa tangazo hilo la NEC, ni wazi kuwa upigaji wa kura ya maoni juu ya Katiba Inayopendekezwa, utafanyika siku chache tu baada ya kukamilika kazi ya uboreshaji wa daftari hilo; na baadaye litatumika kwa uchaguzi mkuu ujao.

Hata hivyo, tume hiyo imeonesha wasiwasi wa kukamilisha kazi hiyo kwa wakati, kutokana na serikali kusuasua kutoa fedha za kufanyia uboreshaji huo, kwani hadi sasa NEC imepatiwa Sh bilioni 15 tu kati ya Sh bilioni 293 zinazohitajika.

Ucheleweshaji wa kutoa fedha hizo, umekuwa ukilalamikiwa na tume hiyo kuwa unachelewesha uboreshaji huo, ambao awali ulikuwa uanze Septemba, lakini umekuwa ukisogezwa mbele kusubiri fedha kutoka serikalini.

Naibu Katibu Mkuu wa Uandikishaji Wapigakura wa NEC, Sisti Cariah alisema hata hivyo wana matumaini makubwa ya kupata fedha zote kwa wakati na kwamba daftari hilo litakamilika ifikapo Aprili 18 na wanatarajia kuandikisha wapigakura milioni 23.9.

“Uandikishaji huu unafanyika kwa haraka ili itakapofika wakati wa kupiga kura za maoni (ya Katiba Inayopendekezwa) daftari liwe limekamilika jambo ambalo tunaamini litakamilika kwa wakati,” alisema.

Juni mwaka huu, NEC ilitangaza kutoa vitambulisho vipya vya kupiga kura nchini kwa wananchi wote, ikiwa ni sehemu ya mchakato wa kuboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura na ungetekelezwa Septemba mwaka huu, kwa kugharimu Sh bilioni 293.

Awali, akitoa taarifa ya uboreshaji wa daftari hilo, Makamu Mwenyekiti wa Tume hiyo ambaye ni Jaji Mkuu mstaafu wa Zanzibar, Hamid Mohamoud Hamid alisema NEC wanaamini watapokea fedha zaidi wakati wanaendelea na uboreshaji huo.
Alisema uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura, ungeanza Septemba mwaka huu lakini haikuwezekana, kutokana na kuchelewa kupatikana kwa fedha kutoka serikalini.

Alisema katika uboreshaji huo, tume imepanga kufanya majaribio ya uboreshaji wa daftari kwa kutumia mfumo mpya wa ‘Biometric Voter Registration’ (BVR) katika majimbo matatu ya uchaguzi nchini, ambayo ni Kawe Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, Kilombero katika Halmashauri ya Mji wa Kilombero na Mlele katika mkoa wa Katavi.

“Kulingana na ratiba ambayo Tume imejipangia, majaribio ya uboreshaji wa daftari yataanza kufanyika katikati ya Novemba mwaka huu na tayari Tume imekwishapokea baadhi ya vifaa muhimu vya uandikishaji ikiwemo Fomu za Uandikishaji na sasa kinachosubiriwa ni kupokea BVR Kits (vifaa) 250 wakati wowote kuanzia leo,” alisema.

Hamid alisema baada ya majaribio kukamilika, itafuatiwa na uboreshaji wa jumla katika maeneo mengine kwa wakati mmoja katika mikoa yote, isipokuwa mkoa wa Dar es Salaam na Zanzibar, ambayo uandikishaji utafanyika baada ya mikoa mingine kukamilika.

Alisema muda wa uandikishaji ni siku saba katika kila kituo na uandikishaji umepangwa kufanyika mwanzoni mwa Januari mwakani hadi katikati ya Februari mwakani katika mikoa yote, isipokuwa Dar es Salaam na Zanzibar, ambapo uboreshaji utafanyika mwishoni mwa Februari mwakani.

Akizungumzia suala la muda wa kura za maoni, alisema kwa sasa wanajikita katika uboreshaji wa daftari kutokana na kuwa tume hiyo, ilishauri serikali kwa sasa daftari la wapigakura kuwa lina kasoro na ingebidi kuboreshwa, kabla ya kufanyika kwa kura ya maoni ya Katiba pendekezwa.

“Tulishauri kuwa ni vyema kura hiyo ingepigwa baada ya kukamilika kwa Daftari, hivyo tunategemea kura hiyo ya maoni itafanyika muda wowote baada ya kukamilika kwa uboreshaji ili haki itendeke,” alisisitiza.

Mbowe wa Chadema ang’aka

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe amesema NEC haijashirikisha vyama vya siasa kwenye mchakato wa kuboresha Daftari la Wapigakura, jambo ambalo linatia shaka utekelezaji wake.

Mbowe alisema vyama vya siasa havijashirikishwa kama wadau kwenye mchakato huo na kwamba taarifa hiyo ya NEC, ndio wanaisikia kutoka kwa vyombo vya habari na kwamba hawana taarifa rasmi.

“Tume haijatushirikisha na jambo hili ni la wadau wote na vyama vya siasa ni wadau wakubwa wa suala hili, sasa kama hatushirikishwi tunasikia tu kutoka kwenu, kwa kweli haya ndio mambo yanayoleta malumbano,” alisema Mbowe alipohojiwa na gazeti hili jana.

Alisema Tume ya Uchaguzi inavyoonekana inawasiliana na chama kimoja cha CCM na kuviacha vyama vingine, wakati mchakato wa uboreshaji Daftari la Wapigakura ni suala la umma, linalopaswa vyama vyote kushirikishwa.

“Uchaguzi huru na haki unaanzia mapema wakati wa uboreshaji wa Daftari la Wapigakura, lakini cha ajabu vyama vya siasa hatushirikishwi kama wadau kutoa mawazo yetu na kisha ndio Tume itangaze kwa vyombo vya habari,” alisisitiza Mbowe.
Kuhusu fedha ambazo NEC wamepata hadi sasa ni Sh bilioni 15, na mahitaji halisi ya uboreshaji daftari hilo ni Sh bilioni 293, Mbowe alisema fedha zilizopatikana ni chache na haziwezi kutosha kufanya utekelezaji. Alisema hawajui Tume ina uhakika gani, kama fedha zinazohitajika, zitapatikana kwa wakati.

Maoni